PUMZIKA KWA AMANI ALBERT MANGWEA ‘NGWAIR’


NIANZE  kwa kuwapa pole wasanii wa muziki na watanzania kwa ujumla, kutokana na msiba wa msanii Albert Mangwea ‘Ngwair’ aliyefariki usiku wa kuamkia Jumanne nchini Afrika Kusini.

Hakika, siku zote msiba uusikie kwa mwenzako, kwani ukiwa kwa jirani unaweza usiwe na maumivu juu ya kile kinachomuumiza.

Lakini, hapo hapo pindi anapofariki mtu maarufu, lazima jamii husika itakuwa imepatwa na mshtuko, ndiyo maana nimeanza kwa kutoa pole kutokana na msiba wa Ngwair.

Ni kweli inauma, lakini chanzo cha kifo cha msanii huyu kinasikitisha sana, hasa baada ya kuthibitishwa kwamba, kimesababishwa na ulevi wa kupindukia.

Jamani, hivi kwa mienendo hii ya wasanii wetu, nchi yetu itakuwa taifa la watu gani, ambao wamekubuhu kwa kutumia mihadarati?

Katika hili, serikali ina wajibu wa kupambana na hao wanaowatumia wasanii wetu kama ndiyo wateja wao wakuu wa biashara hiyo haramu, inayoendelea kuangamiza nguvu kazi ya taifa.

Kama hiyo haitoshi, hata wabunge pamoja na Wizara ya Habari, Utamaduni na Michezo, mna wajibu wa kulisemea hili huko bungeni.

Kwa upande wa wabunge vijana, ambao tayari mko ndani ya mjengo, msifurahie tu malipo na posho mnazopata bungeni, bali mnawajibu wa kuwatetea vijana wenzenu walioko nje ya bunge.

Inauma sana, taifa kupoteza nguvu kazi ya kijana kama ‘Ngwair’, kwani hakuna aliyetaka au kukubali kwamba, msanii huyu amefariki dunia, lakini hivyo ndivyo ilivyo na ukweli utabaki kuwa hivyo.
Ngwair aliyezaliwa mwaka 1982, na jina lake lilikuja juu wakati akiwa na kundi la East Zoo lililokuwa na maskani yake mkoani Dodoma.

Pia, ningependa niupongeza uongozi wa Shirikisho la Muziki wa Tanzania,  chini ya Rais, Ado November ambaye kitaaluma ni Wakili , kwa kuubeba msiba huu, ikiwamo kuurudisha mwili wa marehemu utakaoagwa kesho katika viwanja ama eneo litakalotangazwa baadae na kwenda kuzikwa  mkoani Morogoro.

Wadau mbalimbali wa muziki nchini, wakubwa na wadogo, wameonekana kuguswa na msiba huu na katika hili, wengi wao hasa wanamuziki wakongwe, wamejikuta wakishikwa na kigugumizi na kushindwa kuzungumzia.

Kiukweli, msiba wa Ngwair umenishtua hata mimi binafsi na hata ninapoandika Busati hili, siamini kile kilichotokea, lakini ndiyo imeshakuwa na mapenzi ya Mungu yametimia.

Ngwair, atakumbukwa kutokana na ucheshi, kujituma katika kazi yake ya muziki na kupambana hata pale alipokutana na changamoto mbalimbali, ikiwemo mapromota waongo.

Jambo zuri lingine ambalo litabaki kuwa taswira nzuri na mfano wa kuigwa, ni Ngwair kutokuwa na historia ya kuwa na mifarakano na wasanii wenzake na hii ndiyo sababu kubwa inayowaumiza wengi, hasa waliyofanya naye kazi katika enzi za uhai wake.
Bwana alitoa na bwana ametwaa, jina lake lihimidiwe. Amin.
TANZIA HII IMEANDALIWA NA BONGOWEEKEND.BLOGSPOT.COM

Post a Comment

0 Comments