TUME YA HAKI ZA BINADAMU YAWAFUNDA MAFIA

 

Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora imeendesha mafunzo ya uzingatiaji wa haki za binadamu katika ufikiaji, upatikanaji na usimamizi wa rasilimali za bahari kwa wavuvi wadogo, vikundi vya kina mama wachakataji wa samaki, TAWFA pamoja na BMU.
Mafunzo hayo yaliyofanyika leo Juni 16, 2026 yamelenga kuelewesha jamii kupitia makundi hayo kuhusu uzingatiaji wa haki za binadamu na misingi ya utawala bora.
Akizungumza mara baada ya mafunzo hayo, Afisa Uchunguzi Mkuu kutoka Tume hiyo, Bi. Jovina Mchunguzi ameeleza kuwa mchango wa elimu ya haki za binadamu ni wa wadau wote na si Tume pekee, hivyo wadau wajitokeze kutoa ushirikiano kufikisha elimu.

" Wadau tuungane na Tume katika kufikisha fursa hii kwa wananchi wote, sisi tupo tayari kushirikiana nao " amesema.
Kwa upande wake, Afisa Uvuvi Kilindoni Bi.Jedia Joseph ameeleza kuwa ni matumaini ya Wilaya kuwa mafunzo hayo yataongeza uelewa katika kutambua haki zao na kuleta matokeo chanya kwa kuonesha mabadiliko katika shughuli zao za kila siku.

Mada mbalimbali zimefundishwa ikiwemo haki zilizoainishwa katika katiba, umuhimu wa upatikanaji wa bima za afya kwa wavuvi na wachakataji, hatimiliki za rasilimali za bahari, pamoja na utunzaji wa mazingira katika maeneo ya shughuli za kiuchumi.

"Ninashukuru kupata mafunzo haya, kitu ambacho tulikuwa hatujakipata, tumepata mwamko wa namna gani ya kujihami katika mambo mbalimbali ikiwemo jinsi ya kujitetea pindi haki zetu zinapozuiliwa" alieleza Mzee Silima Juma, Katibu wa kamati ndogo ya hifadhi kutoka kijiji ch Kiegeani.

Post a Comment

0 Comments