GEREZA KWAMNGUMI LAKABIDHI ALIYEKUWA MFUNGWA VIFAA VYA UJENZI



Na Ssgt Mawazo Mtondo 

Mkuu wa Gereza la Kwamngumi mkoani Tanga, Mrakibu wa Magereza (SP) Francis Makelemo, Agosti 11, 2026, aliongoza zoezi la kumkabidhi aliyekuwa mfungwa, Ndugu Tumaini Mahuji, vifaa mbalimbali vya ujenzi baada ya kumaliza kutumikia kifungo chake katika Gereza hilo.

SP Makelemo amesema Jeshi la Magereza limeendelea kuwa chuo cha mafunzo kwa kuwapatia wafungwa fursa ya kupata elimu, ujuzi na maarifa ya ufundi stadi, pamoja na vitendea kazi vinavyowawezesha kujitegemea na kuendesha maisha yao wanaporejea katika jamii.

Vifaa alivyokabidhiwa ni pamoja na pima maji, msumeno wa mbao, nyundo, tape measure, kobilo, koleo na sululu.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji wa Korogwe, Bw. Ally Mkwavinga, alisema juhudi zinazofanywa na Jeshi la Magereza katika kuwajengea wafungwa uwezo na kuwapatia ujuzi ni muhimu katika kuwaandaa kurejea katika jamii wakiwa na uwezo wa kujitegemea.

Katika hafla hiyo, Ndugu Tumaini Mahuji alitoa shukrani kwa serikali na uongozi wa Jeshi la Magereza kwa kukabidhiwa cheti kutoka Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA), pamoja na vifaa mbalimbali vya ujenzi vitakavyomsaidia kutumia ujuzi alioupata kujipatia kipato na kujikimu yeye pamoja na familia yake.

Post a Comment

0 Comments