MSEMO WA WAMAKONDE, KILA MUNU AVE NA KWAO WATUA SWEDEN

 


Bendi ya muziki ya Tongolanga iliwahi kuimba “kila munu ave na kwao ”ikimaanisha kila mtu awe na kwao, ujumbe kutoka Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro uko Sweden kuwaeleza wananchi wa taifa hilo kuwa asili yao kama binadamu wengine ni Ngorongoro na kuwakumbusha warudi nyumbani kwao.

Akizungumza katika maadhimisho ya siku ya kiswahili duniani Stockholm Sweden Afisa Uhifadhi Mkuu anayeshughulikia masoko bw. Michael Makombe amesema Ngorongoro ina ushahidi wa kisayansi unaothibitisha kuwa binadamu wa kale aliyesimama na kutembea kwa miguu yake miwili takribani miaka milioni 3.6 iliyopita alipatikana Ngorongoro.

“Karibuni sana nyumbani Tanzania, karibuni Ngorongoro ambapo kisayansi ndio eneo lenye ushahidi unaonesha zaidi ya miaka milioni 3.6 iliyopita binadamu wa kale alianza kutembea kwa miguu miwili katika eneo la Laetoli zilipogundulika Nyayo za binadamu wa kale ”,alisema bwana Makombe.

Baadhi ya wageni waliotembelea katika banda la Ngorongoro kwenye maadhimisho ya siku ya kiswahili nchini humo walieleza jinsi wanavyosikia taarifa hizo kupitia vitabu vya historia na kushauri kuongeza nguvu kwa watanzania kuhifadhi historia hiyo.

“Haya ni maajabu makubwa kwetu, natamani siku moja nifike Ngorongoro kuona asili yangu na hapo binadamu alipoanza kutembea kwa miguu miwili”,alisema bwana Georgen Stelingmen mkazi wa jiji la Stockholm.

Maadhimisho ya siku ya kiswahili duniani yaliyofanyika katika ngazi ya ubalozi nchini Sweden yalikuwa na hamasa kubwa kutokana na wageni wengi kutaka kujua jinsi ya kutembelea vivutio vya utalii vilivyopo hifadhi ya Ngorongoro.

Post a Comment

0 Comments