WATANZANIA WAPONGEZWA KUWAPUUZA 'MADALALI' WA MAANDAMANO

Na Mwandishi  Wetu,  Zanzibar 

Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimesifu msimamo wa  watanzania kwa   kuwapuuza mamluki na vibaraka wachache  wanaotumiwa na mabeberu kuvuruga ustawi wa amani, umoja na mshikamano  wa kiTaifa. 

Kimekitaja  kitendo cha wananchi  kuonyesha utii wa sheria na kutojitokeza katika maandamano haramu ya 09 Desemba 2025,   kimefikisha ujumbe kuwa waTanzania kamwe hawatagawanyika

Katibu wa Kamati  Maalum ya NEC Zanzibar, Idara ya Itikadi, Uenezi na Mafunzo,  Khamis  Mbeto  Khamis, ameeleza hayo na kuwataja waTanzania walikataa, wamekataa na wataendelea kukataa kuuza utu wao au kupoteza heshima ya Taifa lao.

Mbeto aliwashukuru  waTanzania  kwa uamuzi huo unaodumisha  amani na utulivu,  ukiwasuta vibaraka  wanaonunulika kwa ujira wa fedha zenye  dhambi ili  wachochee machafuko nchini.

Alisema njia pekee bora na sahihi ni  serikali  kuendelea na mkakati wake wa kuzitafutia tiba changamoto zinazowakablii wananchi,  kuboresha huduma za jamii na kupata mbinu  mbadala zitakazotanua wigo wa ajira kwa vijana. 

"Watanzania kwa umoja na  mshikamano wao wamewatumia ujumbe vibaraka wachache waliodhani wangefanikiwa  kuwagawanya.

Kwa nguvu  ya  uzalendo, uTaifa walionao, wamechagua   kulinda heshima na kukataa kugawanyika" alisema Mbeto.

Katibu  huyo Mwenezi  aliongeza kusema  kwa namna  yeyote ile, waTanzania wataendelea  kuthamini Taifa lao, umoja wa kitaifa wa nchi zao kwani wamekuwa wakiishi kwa maelewano  kwa miaka zaidi  ya sitini.

"Ahadi  na kazi ya CCM ni kuzisukuma serikali zitekeleze wajibu wa kisera kwa kuzipatia majibu chanya changamoto zote. CCM iko tayari  wakati wowote  kumaliza utata  wowote kwa njia ya majadiliano na mazungumzo mezani "alisema. 

Alimtaja Mwenyekiti  wa CCM, Rais Dkt. Samia Suluhu  Hassan ni kiongozi  shupavu, msikivu, muungwana, anayeshaurika hivyo yuko tayari wakati  wowote  kushughulikia matatizo kwa njia za kistaarabu. 

Katibu huyo Mwenezi   aliwataka waTanzania  kusoma mienendo  hatarishi iliozikumba na inayoendelea kuzitatiza baadhi ya nchi na mizozo yake imeacha vita, mapigano na machafuko yasiokwisha.

"Watanzania tukatae ghiliba na ushawishi  utakaovuruga amani na utulivu. Tuwe tayari  kujadili changamoto  kwa njia za wazi bila kuvutana mashati. Thamàni ya amani, umoja na utulivu haiuzwi mahali popote duniani " alisema  Mbeto.

Post a Comment

0 Comments