Mwenyekiti Kamati ya Taifa ya Maridhiano nchini Sheikh Alhad Mussa ameiasa jamii kuacha tabia ya kuhukumu mtu , hakuna kifo kibaya kama mtu kuondoka ghafla unakwenda 'fresh'bila kuomba toba kwa mola wako lakini muumini yeyote anayeumwa kwa muda mrefu hupata muda wa kutubu na kurejea kwa mola wake.
Alhad Mussa amesema hayo tarehe 21 Aprili 2025 alipokua akitoa mawaidha kwa waombolezaji waliofika Bunju nyumbani kwa aliyekua Mkurugenzi wa Kampuni ya Lino International Agency marehemu Hashim Lundenga 'Uncle Hashim' ambapo mwili wake umesafikishwa na kuzikwa leo tarehe 23 Aprili 2025 Kidatu Mkoani Morogoro.
"Tuache tabia za kutoa hukumu kwa wenzetu pindi wanapotangulia mbele ya haki kwa sababu mandiko matakatifu ndani ya Qur ani tukufu yanasema kuwa kuumwa ni ibada hivyo mtu anapoumwa kwa muda mrefu Mwenyeezi Mungu humsafisha madhambi yake na pia hupata muda wa kutubu kadhalika ifahamike kwamba hakuna dhambi kubwa ama isiyosameheka mbele ya Mwenyeezi Mungu na hakuna anayejua mja anapoomba toba kwa muumba wake hiyo siri ya baina ya wao wawili" amesema Alhad Mussa.
"Uislamu ni dini ya mazingatio na fikra mwanaadamu anatakiwa awe na mazingatio katika mambo makubwa hasa kifo , tumekua tukiwasindikiza ndugu zetu lakini tunakosa mazingatio ya kifo na kusahau kuwa kila aliyezaliwa na mwanamke hata akiishi maisha mazuri na marefu kiasi gani iko siku atakufa" .
"Kifo kina kata ladha ya kila kitu , mkeo,mumeo, watoto na mali zako vyote utaviacha na utaondoka maiti huwa vinamfuata vitu vitatu viwili hua vinarudi ambavyo ni ndugu , na jamaa watoto na mali zake vitarudi na wala hakuna ndugu au mtoto atasema nizikwe naye ila kinachobaki pale ni amali njema , matendo mema je mahusiano yako na Mungu yakoje unaishije na wenzako , je unaabudu Mungu pamoja na neema za pumzi na afya na kunshukuru Mungu kwa kumuabudu ? jihesabuni nafsi zenu kabla hamjahesabiwa je una shukrani za pumzi na mali alizokujaalia Mungu?
Ishi na watu wote kwa tabia nzuri bila kujali dini, sisi wanadamu tunapoishi tunapitia mambo mengi sana mwanadamu kutenda dhambi ndiyo ubinaadamu na waliobora kwa binaadamu ni kwa wale wanaotubia.
Mwenyeezi Mungu hatuonei taabu tunapotenda dhambi ila baada ya dhambi tubia , Mwenyeezi Mungu anawapenda wenyekutubia dhambi zao na kujitwaharisha na kukiwa na mtu hapa hajatenda dhambi basi huyo ni Malaika sababu wao hawamuasi Mwenyeezi Mungu siku zote wanafanya yale mema waliyoamrishwa na Mungu.
"Mlango wa toba uko wazi huo ndiyo ukumbusho na tuwe tunatoa faraja maana kuna viongozi huwa wanatoa mawaidha makali usiwakatie tamaa waja wa Mwenyeezi Mungu milango ya pepo iko wazi wewe unawafungia milango ya peponi kama pepo ya babaako na toba kati ya mola na mja wake Mwenyeezi Mungu anasemsa rehema zake zimeenea kwenye kilakitu" amesema Alhad Mussa.
Mkurugenzi wa Bodi ya Utalii nchini Ephraim Mafuru akimuelezea marehemu Lundenga amesema kuwa ataendelea kumkumbuka kutokana na nguvu yake ya ushawishi siyo tu kwa wasichana warembo bali hata kwa wadhamini katika Kampuni mbalimbali ambapo alikuwa na nguvu ya kutoa ushawishi na kuweza kupata udhamini mnono kwa kuanzia ngazi ya vitongoji hadi taifa.
Meneja wa zamani wakinywaji cha Pilsner Ice waliowahi kutoa udhamini mnono katika shindano la Miss Tanzania David Minja amesema kuwa "wote tunajua pengo ambalo tasnia ya ulimbwende imepata na alama kubwa ambayo Lundenga ameiacha kwa taifa japo hakufanya mwenyewe alikuwa na jopo la watu wengi nyuma yake pamoja na warembo walioshiriki ,kwangu mimi tasnia ya urembo ilikua ni ngazi ya kuwajenga kina mama shupavu na viongozi bora katika jamii hilo liko wazi hivyo itoshe kusema apumzike kwa amani na tuendelee kumuezi" amesema Minja.
Akizungumza na kutoa salamu za pole kwa niaba ya warembo wote waliopita katika jukwaa la la Miss Tanzania Faraja Kotta Nyarandu (Miss Tanzania 2001)amesema kuwa "Anko Hashim Lundenga amegusa wanawake wengi kwa kupitia yeye tumeweza kuvumbua vipaji mbalimbali kwa kuwa jukwaa la Miss Tanzania lilikua ni tanuri kwa walimbwende nchini Lundenga alikua baba mlezi, rafiki na kama kiongozi ambaye amegusa maisha ya warembo nchini ambapo wameweza kutimiza njozi zao katika maisha" amesema Faraja.
"Miss Tanzania ni tanuru lililotupa chachu kwa kila mmoja wetu na katika kumbukumbu ya kila mwanamke ambaye alipita kwenye jukwaa la Miss Tanzania amesimama imara katika eneo lake"amesisitiza Faraja .
Mwili wa marehemu Lundenga ukiwasili nyumbani kwake Bunju Jijini Dares Salaam jana tarehe 21 Aprili 2025 .
Baadhi ya warembo walioshiriki shindano la ulimbwende la Miss Tanzania katika miaka tofauti wakiwa waliofika msibani wakiwa katika picha ya pamoja.
Mwili wa marehemu Anko Hashim Lundenga ukisaliwa Salat jeneza kijijini kwao kabla ya mazishi yaliyofanyika leo tarehe 22 Aprili 2025 Kidatu Mkoani Morogoro.
Hakika sisi ni wa Mwenyeezi Mungu na kwake tutarejea (Innalilah Wainna Ilaih Rajioun).









0 Comments