KISHINDO CHA DKT. KIJAJI MAMLAKA YA HIFADHI YA NGORONGORO.

 

Na Kassim Nyaki, Arusha.

Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb) leo tarehe 29 Januari, 2026  Jijini Arusha amezindua bodi ya wakurugenzi wa Mamlaka ya hifadhi ya Ngorongoro (NCAA) na kuielekeza kusimamia uhifadhi, kubuni mazao mapya ya utalii na kuyatangaza na kuboresha huduma za maendeleo kwa wananchi wa wilaya ya Ngorongoro.

Dkt. Kijaji amebainisha kuwa hifadhi ya Ngorongoro ni eneo muhimu kiuhifadhi na moja ya maeneo yanayotambuliwa kama urithi wa dunia na UNESCO hivyo ameiunda bodi hiyo kwa kuteua manguli wa kila sekta ili kufikia matamanio ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt, Samia Suluhu Hassan ya kuona uhifadhi, utalii na maendeleo ya jamii vinasimamiwa bila kuipoteza hifadhi hiyo.

“Nimeteua wataalam kutoka sekta zote serikali na binafsi ili muisaidie serikali katika kusimamia maeneo hayo kwani hifadhi ya Ngorongoro ina mvuto mkubwa duniani,hivyo ni jukumu lenu kutumia taaluma na weledi wenu katika kuhakikisha Ngorongoro inaendelea kuwa na tija kwa taifa”,alisema Waziri Kijaji.

Ubobezi wa wakurugenzi wapya wa bodi ya Ngorongoro na umahiri wao kitaaluma ulielezwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii Dkt.Hassan Abbasi ambaye alisema kazi ya kuwateua wakurugenzi hao wa bodi haikuwa rahisi kutokana na uchambuzi yakinifu uliofanywa ili kupata watu ambao watakuwa msaada kwa hifadhi hiyo na taifa kwa ujumla.


Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Mamlaka ya hifadhi ya Ngorongoro ambae ni Mkuu wa Majeshi mstaafu Jenerali Venance Mabeyo amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa kumteua tena kuongoza bodi hiyo kwa kipindi kingine cha miaka mitatu na kumpongeza waziri wa Maliasili na Utalii kwa kuteua watu wenye taaluma tofauti na kuwataka wakurugenzi hao kuacha alama kama ilivyokuwakwa wakurugenzi wa bodi iliyopita.

Wakurugenzi wapya wa bodi wa mamlaka hiyo wamebobea katika sekta ya uhifadhi, utalii, fedha na uchumi, utawala, sheria, diplomasia,utawala bora, maendeleo ya jamii, ukaguzi na teknolojia ya mifumo ambapo pia wana uzoefu mkubwa katika utumishi wa serikali na sekta binafsi hivyo kutoa mwanga wa kutosha katika kuimarisha mamlaka hiyo.

Mapema Kamishna wa Mamlaka ya hifadhi ya Ngorongoro bwana Abdul-Razaq Badru alivishwa cheo na kuapishwa rasmi kuwa kamishna wa mamlaka hiyo na kuahidi kuendelea kuchapa kazi kwa weledi na uaminifu wa hali ya juu ili kuimarisha majukumu ya Ngorongoro ambayo ni uhifadhi, utalii na maendeleo ya jamii.

Post a Comment

0 Comments