RC KUNENGE AFUNGA KONGAMANO LA VIJANA KUHUSU UMUHIMU WA KUSHIRIKI MBIO ZA MWENGE


Mkuu wa Mkoa wa Pwani Abubakari Kunenge amewataka vijana kuwa wazalendo na wasiamini kushindwa kwenye jambo lolote wanalotaka kulifanya katika kujiletea maendeleo na kutimiza ndoto zao.

Kunenge ameyasema hayo leo tarehe 29 Machi  2025  kwenye Ukumbi wa Bertil Melin uliopo Shirika la Elimu Kibaha wakati wa akifunga  Kongamano la Vijana juu ya umuhimu wa kushiriki Mbio za Mwenge wa Uhuru. 

RC Kunenge amesema kuwa vijana wanapaswa kujifunza  kupitia kwa Rais  wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Dkt Samia Suluhu Hassan ambaye ameonesha umahiri katika kutekeleza miradi mbalimbali nchini kwani baadhi ilikuwa ni ya muda mrefu lakini amepambana na kuikamilisha  baadhi ya miradi na mingine ikikaribia kukamilika ikiwemo ya Daraja la mto Wami, Daraja la Kigogo Busisi na Bwawa la maji la Kidunda.

Amesema kuwa vijana wanapaswa kuwa wazalendo na watu wajifunze kupitia kwao hivyo wanapaswa kutengeneza vitu vya kipekee haijalishi hawana uzoefu au la.

Ameongeza kuwa vijana wajiajiri wasisubiri kuajiriwa kwani mchango wao ndani ya jamii na Taifa ni mkubwa na kila jambo linawezekana ambapo tulipoambiwa tutaandaa uzinduzi mbio za mwenge hatukuwa na uwanja lakini sasa upo na tumefanikiwa.

Baadhi ya wanafunzi wakiwa kwenye Kongamano hilo.

Kwa upande wake Mratibu wa Kongamano hilo Omary Punzi amesema kuwa vijana hao wamefundishwa mambo mbalimbali ikiwemo umuhimu wa vijana kushiriki kwenye mwenge.

Punzi amesema kuwa mwenge ni moja ya Tunu za Taifa ambapo zimeanzishwa na waasisi wa Taifa letu ambazo zinapaswa kuenziwa kwa ajili ya kuleta maendeleo ya nchi. 

Kongamano hilo lilikuwa la siku mbili ambapo lilianza jana ikiwa ni maandalizi ya mbio za mwenge wa uhuru unaotarajiwa kuzinduliwa Aprili 2 mwaka huu kwenye uwanja wa Shirika la Elimu Kibaha Tumbi ambapo mgeni rasmi anatarajiwa kuwa ni Makamu wa Rais Dk Philip  Isdor  Mpango.

Post a Comment

0 Comments