TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI KUTOKA TFF

                     PINGAMIZI DHIDI YA MWAKINGWE
Klabu ya Majimaji ya Songea imeliandikia Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) ikiondoa pingamizi ililoweka awali dhidi ya mchezaji Ulimboka Mwakingwe ambaye Simba imemuombea usajili kwa msimu wa 2011/2012.
Majimaji kupitia Katibu Mkuu wake Henry Kabera imesema baada ya kukutana na uongozi wa Simba imeamua kuondoa pingamizi dhidi ya mchezaji huyo ambaye ilimsajili kwenye dirisha dogo msimu uliopita.
Awali Majimaji iliwasilisha pingamizi TFF kwa wachezaji wake kumi na moja (11) iliosema kuna tetesi wamesajiliwa na klabu mbalimbali za Ligi Kuu ya Vodacom, lakini hawajafanyiwa uhamisho ingawa bado wana mikataba na timu hiyo.
Wachezaji hao ni Said Mohamed (Yanga), Ulimboka Mwakingwe (Simba), Ally Bilaly (Villa Squad). Pia wapo Juma Mpola (Kagera Sugar), Evarist Maganga (Villa Squad), Kulwa Mobby (Polisi Dodoma), Paul Ngalema (Ruvu Shooting), Mohamed Mpola, Lulanga Mapunda (Toto Africans), Hamad Waziri na Yahya Shaban Haruna.
U23, SHELISHELI WAINGIZA MIL 5/-
Mechi ya kirafiki ya kimataifa kati ya timu ya Taifa ya vijana wenye umri chini ya miaka 23 na timu ya Taifa ya Shelisheli iliyochezwa jana Uwanja wa Kumbukumbu ya Sheikh Amri Abeid Kaluta jijini Arusha imeingiza sh. 5,014,000.
U23 ilishinda mechi hiyo mabao 3-1. Timu hizo zitarudiana tena kesho (Julai 29 mwaka huu) kwenye uwanja huo huo. Shelisheli iko kwenye ziara ya maandalizi ya michuano ya nchi za visiwa ziliko katika Bahari ya Hindi barani Afrika itakayofanyika mwezi ujao. Visiwa hivyo ni Shelisheli, Mauritius, Comoro, Mayotte, Reunion na Madagascar.
Julai 30 mwaka huu, kocha wa Taifa Stars, Jan Poulsen ambaye yuko Arusha kushuhudia mechi hizo atatangaza kikosi cha Stars ambacho Agosti 7 mwaka huu kitakwenda Palestina kucheza na timu ya Taifa ya nchi hiyo katika mechi itakayofanyika katika kalenda ya FIFA- FIFA dates (Agosti 10 mwaka huu).
Boniface Wambura
Ofisa Habari
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)

Post a Comment

0 Comments