Na Mwandishi Wetu
Tanzania imepata nafasi 150 za ufadhili wa masomo nchini Algeria kwa wanafunzi waliofanya vizuri, ikiwa ni sehemu ya juhudi za Serikali kuongeza fursa za elimu ya juu nje ya nchi.
Akizungumza na waandishi wa habari Septemba 11, 2026 jijini Dar es Salaam, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda, amesema Serikali ya Algeria itagharamia ada za masomo, huku Tanzania ikigharamia fedha za kujikimu kupitia utaratibu wa Samia Scholarship.
Amebainisha kuwa fursa hiyo ni mwendelezo wa mkakati wa Serikali wa kuongeza nafasi za masomo ya elimu ya juu nje nchi, ambapo kati ya wanafunzi 1,000 waliotangazwa kupata Samia Scholarship, wanafunzi 10 wamechaguliwa kwenda Moscow, Urusi.
Aidha, ameongeza kuwa majina ya wanafunzi 150 watakaochaguliwa yatawekwa kwenye tovuti ya Wizara www.moe.go.tz pamoja na maelekezo ya hatua za kuwasilisha nyaraka na taratibu za safari, ikiwemo upatikanaji wa hati za kusafiria.
Prof. Mkenda amesema Serikali inalenga kuhakikisha fursa hizo zinawanufaisha wanafunzi kutoka makundi mbalimbali, wakiwemo watoto wa wakulima na wafugaji, huku wanafunzi watakaokwenda Algeria wakitakiwa kuwa tayari kujifunza lugha ya Kifaransa, inayotumika katika sehemu kubwa ya masomo nchini humo.
Akizungumza mara baada ya tangazo la Waziri, Balozi wa Tanzania nchini Algeria, Mobhare Matinyi, aliishukuru ya Algeria kwa kutoa nafasi nyingi mwaka huu kuliko miaka mingine na kuonesha matumaini kwamba mwakani zitaongezeka zaidi.
"Mwaka jana Algeria ilipokea wanafunzi wa Tanzania 45 lakini mwaka huu kutokana na mpango wa Samia Scholarships inayosimamiwa na Wizara ya Elimu wanakuja 150," alisema Balozi Matinyi.
Balozi aliongeza zaidi kuwa Algeria umepiga hatua kubwa katika elumu ya juu na kila huzalisha wataalam wa aina mbalimbali na hivyo Serikali kupitia Ubalozi uliomba nafasi zaidi ili izitumie kupata wataalam kwenye maeneo mbalimbali ya sayansi kama kilimo, afya, taarifa (data science) na pia kwenye teknolojia, hususani katika Teknolojia ya Habari na Mawasiliano.


0 Comments