Social Icons

Saturday, February 25, 2017

RAIS MSTAAFU DKT. JAKAYA KIKWETE AKUTANA NA RAIS ALASSANE OUATTARA JIJINI ABIDJAN

Rais Mstaafu na Mjumbe Maalum wa Kamisheni ya Kimataifa ya Elimu, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete jana tarehe 23Februari 2016 amekutana na kufanya mazungumzo  na Rais wa Ivory Coast, Mhe. Alassane Ouattara katika Ikulu yake jijini Abidjan.. Mazungumzo hayo yalihudhuriwa pia na Makamu wa Rais, Waziri wa Fedha na Waziri wa Elimu.

Katika mazungumzo yao, Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete na mwenyeji wake Rais Ouattara wamezungumzia hali ya elimu bara la Afrika na Ivory Coast kwa ujumla na haja ya kufanya mageuzi makubwa katika elimu ili kuweza kuendana na kasi ya nchi zilizoendelea.

Rais Mstaafu Kikwete amempongeza Rais Outtara kwa jitihada kubwa anayoifanya kuinua elimu nchini mwake. Kwa mujibu wa utafiti wa Kamisheni, Ivory Coast iko katika nafasi nzuri ya kufikia viwango vya juu vya ubora wa elimu vya nchi zilizoendelea iwapo itaongeza juhudi ya kufanya mageuzi kulingana na mapendekezo ya Kamisheni hiyo.

Rais Outtara amemuhakikishia Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete azma ya nchi yake kufanya mageuzi makubwa katika sekta ya elimu nchini mwake. Ameelezea utayari wa nchi yake kujiunga na mpango huo wa kufanikisha mapinduzi ya sekta ya elimu ndani ya kizazi kimoja ifikapo mwaka 2040.

Akiwa jijini Abidjan, Rais Mstaafu ametembelewa na viongozi wa Watanzania wanaofanya kazi Benki ya Maendeleo ya Afrika na Watoto  wa Watanzania hao ambao walitaka kujua kuhusu masuala ya uongozi na maisha baada ya kustaafu. 
 Rais Mstaafu na Mjumbe Maalum wa Kamisheni ya Kimataifa ya Elimu  Dkt. Jakaya Kikwete akikaribishwa na Rais Alassane Ouatara wa Ivory Coast jijini Abidjan katika Ikulu ya nchi hiyo.
Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Kikwete akimkabidhi ripoti ya 'Kizazi cha Elimu' Rais Allasane Ouatarra wa Ivory Coast
 Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Kikwete akizungumza na Waandishi wa Habari baada ya mazungumzo na Rais Alassane Ouattara. Kulia kwake ni Makamu wa Rais wa nchi hiyo Mhe. Daniel Kablan Duncan
 Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Kikwete akiagana na Rais Alassane Ouattara baada ya mazungumzo yao   Ikulu ya Ivory Coast.

 Rais MStaafu Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete katika picha ya pamoja na Uongozi wa Watanzania wanaofanya kazi Benki ya Maendeleo ya Afrika jijini Abidjan
 Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Kikwete akifurahia mazungumzo na baadhi ya watoto wa Watanzania waishio Ivory Coast waliomtembelea hotelini kwake Abidjan
Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Kikwete akiwasainia autograph  watoto waliomtembelea hotelini kwake  jijini Abidjan.

No comments:

 
 
Blogger Templates