Social Icons

Wednesday, August 24, 2016

LILIAN 'INTERNET' AITA MASHABIKI MANGO GARDEN J'MOSI AKAWAAMBIE BAIBAI



Lilian Tungaraza 'Internet' akiwa katika pozi . 

Imezoeleka  kuona mtu akiagwa pale anapostaafu kazi serikalini, kwenye sekta binafsi na kwingineko, na pia hivi sasa ni sawa na jambo la kawaida kuona msanii akipotea kutoka kwenye steji na anapotafutwa inaelezwa kwamba alishaacha usanii.

Lakini kwa mara ya kwanza katika tasnia ya unenguaji nchini, uongozi wa kampuni ya  African Stars Entertainment (ASET) inayomiliki bendi ya Twanga Pepeta, umeandaa  usiku maalum wa kumuaga mnenguaji wake mahiri, Lilian Tungaraza, yule ambaye ni maarufu zaidi kwa mashabiki wa ‘minenguo’ nchini kama Lilian Internet. 

Akizungumza katika mahojiano maalum na  Bongoweekend  jijini Dar es Salaam, Internet anasema ameamua kuacha unenguaji kwa ridhaa yake mwenyewe na kutoka moyoni, hivyo hakuna yeyote aliyemshurutisha kwa namna moja ama nyingine. 

“Nimeamua kuacha kutokana na umri wangu kuwa mkubwa, hivyo nawaachia hawa (vijana kama) kina Stella na wengineo waendelee na kazi hii.  Kwa hiyo natarajia kuwa onyesho langu lililopangwa kufanyika Agosti 27 mwaka huu (ambayo ni Jumamosi wiki ijayo) kwenye Ukumbi wa Mango Garden litakuwa la kukumbukwa”, anasema.

“Mimi ndiye nilimfuata Mama Asha Baraka na kumweleza kuwa sasa ninahitaji kupumzika ili niwapishe wengine kwa sababu huu ni wakati wa mabadiliko, siyo kwmba nimeshindwa kazi (hii) ya kunengua ila nimeamua nistaafu”, ana ainisha.

Anaongeza kwamba bado yuko ‘fiti’ kwa namna zote kwenye steji kiasi kuwa hata leo akiamua kupanda wenzie wanafahamu jinsi atakavyowaonyesha kazi, lakini hatimaye uamuzi wake wa kupisha kando ndiyo huo.

Internet ambaye ubora wake wa kunengua umempa jina kubwa ‘Tizedi’ anabainisha kuwa amekuwepo stejini kwa miaka 19 hivi sasa, hivyo ana mambo mengi ya kuweza
kumfanya awe kocha wa madansa ikiwemo kuwapa ushauri wake.

 Nini kilichomvutia kunengua ?

Anasema alianza muziki kwa kuvutiwa na ‘masisteri’ wawili ‘mapacha’ waliokuwa wanenguaji ‘staa’ wa miondoko ya Nzawisa kutoka nchi iliyokuwa Zaire wakati huo, ile ambayo sasa inaitwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), Scola Miel na Betty Sumbu.

Mabinti hao kwa pamoja walikuwa katika kundi la L’Anti Choc likiongozwa na Abuobakari Mbenzu Ngombani, yule ambaye wengi humuita kuwa Bozi Boziana. 

Bila shaka anazungumzia kipindi kile cha L’Anti Choc  ya Response ya Lipapa ya Wara. Anazungumzia kipindi kile ambacho kundi hilo ‘lilitesa’ na vibao vitamu na maridadi kama ‘Tembe na Tembe, Doukoure, Evelyn, Penitencier, Chama Chiko, Bissalu, Ebale, Lucky’ na ‘C’est Pas Comme Ca’ vinavyobeba albamu ile ‘kali’ ya ‘Tembe na Tembe’.

“Nilikuwa najifungia ndani ninaangalia mikanda yao ya video na baada ya hapo nikitoka nacheza staili zao zote bila ya kukosea, jambo lililosababisha niwe nakwenda kucheza kwenye shughuli mbalimbali kama harusi, kipaimara na nyinginezo”, anasema alivyoanza mpaka kuwa mahiri kabisa wa kunengua stejini.

Akiwa katika harakati zake hizo ndipo jirani yake mmoja aliyeitwa Mama Sanda aliyekuwa mkubwa kuliko yeye alipomshawishi siku moja kwenda naye kwenye ukumbi wa Silent Inn, Mwenge jijini Dar es Salaam.

Anasema ilipofika ‘ofa’ ya watoto ‘kuidandia’ steji ili kuonyesha vitu vyao ndipo nyota yake ikang’ara. Alicheza kwa namna zote mahiri na kumvutia mwanamuziki aliyekuwa kiongozi wa bendi ya Ikibinda Nkoi wakati huo, Ellystone Angai.

“Angai aliniita kando akaniambia amenikubali, hivyo akaniambia niwe nakwenda kila Jumapili ambako bendi hiyo huwa inapiga dansi la watoto na mimi nikaona hapahapa ndiyo njia, hivyo nikaitumia bila kufanya ajizi”, anakumbuka vyema.

Anasema kipindi hicho cha mwaka 1998 alikuwa bado na miaka 17 tu, lakini aliamua  kujikita zaidi katika bendi hiyo iliyokuwa na wanenguaji wengine mahiri kama Salma Abeid, Mamii Korando na wengineo.

Pamoja na kipaji alichokuwa nacho, Lilian anasema bado alikuwa akienda kwenye maonyesho ya bendi hiyo kwa kujificha bila kuruhusiwa na mama yake, lakini hatimaye akagundulika baada  ya kituo cha televisheni cha ITV kurusha  maonyesho  ya bendi hiyo.

“Hapo mama yangu akaniambia kumbe wewe ndiyo maana umekataa kusoma kwa sababu ya muziki? Haya endelea na hicho unachotaka na mimi nikaacha rasmi shule na kujikita katika unenguaji wa bendi”, anasimulia. 

Ilipofika mwaka 2001, Lilian alijiunga na bendi ya African Stars na miondoko yake ya Twanga Pepeta ambako safu yao ya unenguaji ilikuwa ikiundwa na yeye mwenyewe, Aisha Madinda na Halima White wote hao  hivi sasa ni marehemu.

Amefaidika na nini kutokana na kazi hiyo?

“Tukizungumzia tasnia ya sanaa kuna faida nyingi nilizopata. Kwanza kabisa nimeweza kuisaidia familia yangu akiwemo mama yangu na wadogo zangu, nimepata mume na watoto wawili. Nimeweza kuendesha maisha yangu mwenyewe”, anajibu kwa utulivu na umakini mkubwa na kuendelea:

“Pia kwa kupitia muziki nimekuwa ni miongoni mwa wasanii waliobahatika kwenda nchi mbalimbali kulikokuwa kunafanyika matamasha ya muziki kama Oman, Dubai, Kenya, Uganda, Uingereza, Uholanzi, Sweden na Norway ambako nimekwenda kwa sababu tu ya unenguaji”.

Anasemaje kuhusu Twanga Pepeta?

“Nawashkuru ‘staff’ wote kwani nimeishi nao vizuri  bila kumsahau mama ambaye ni Mkurugenzi wake (akimaanisha Asha Baraka).  Amenilea, ameniozesha. Nashukuru kwamba nimekaa naye vizuri kwa muda wote huo”, anasema.

Nasaha kwa wanennguaji wenzake 

Maisha ni kupigana, bila hivyo hakuna lolote linaloweza kusogea. Lazima kuwepo pia na ubunifu, wasitegemee uongozi kwamba ndio utoe maelekezo kwa ajili ya manufaa ya bendi. Mawazo mapya yanatakiwa kwa sababu yatasaidia kupata mishahara pamoja na posho za kujikimu”, anawaasa wanamuziki wanaobaki katika bendi hiyo iliyodumu kwa miaka mingi kati ya zote zinazotamba na miondoko inayoitwa kuwa ya ‘bolingo’. 

Kana kwamba haitoshi, Lilian anataka wasanii wote wajitume zaidi kwa vile kupata jina siyo kitu cha mchezo. “Binafsi nimepewa jina hili la Internet, sikulipata hivihivi ila nilijituma. Kuna vitu vingi ambavyo msanii hupitia na yapo mazuri na mabaya, hivyo kwa kuwa na mimi ni kioo chao wachukue mazuri yangu na kuacha mabaya”, anasema.

Changamoto alizoziona

Akizungumzia changamoto zinazowakabili wanenguaji anasema zipo nyingi ikiwemo jamii kuwadharau kwa kuona kwamba hawafai, lakini yeye binafsi hajali akisema kuwa amefanya mambo mengi kutokana kwa sababu ya kunengua stejini.

“Kwenye muziki sisi wacheza shoo tunadharaulika sana na mimi mwenyewe nimewahi kutukanwa na mtu ‘live’ na wanaume ndiyo wanaongoza. Utaona wakati wa kukutunza hakupi pesa mkononi, atakuwekea katikati ya makalio”, anasema kwa huzuni.

Akifafanua kuhusu wanavyovaa wanenguaji, Lilian anasema kuwa mavazi yao ni ya stejini na ya kikazi peke yake, lakini hawawezi kuvalia hivyo wanapokuwa sehemu nyingine za kawaida huku akiongeza kwamba pindi wanaposhuka tu kutoka kwenye jukwaa, kila mtu aanendelea na maisha yake ya kawaida yakiwemo majukumu ya kifamilia. 

“Hivyo ninachoweza kusema ni kwamba sitakuwa mbali na masuala ya muziki. Ninaweza hata nikaanzisha kikundi changu cha madansa ambao nitawafundisha kucheza na baadaye watakuwa wakitumika kwa mambo tofauti”, anasema. 

Naye Mkurugenzi na mmiliki wa bendi hiyo, Asha Baraka  anasema kuwa tayari mashabiki wa Twanga Pepeta wamepewa taarifa za onyesho hilo maalum, hivyo akaomba wadau mbalimbali wajitokeze kwa wingi, Jumamosi wiki ijayo ili waweze kumuaga Lilian huku akisema kwamba kutakuwa na mambo kadhaa ya kushtukiza. 

“Internet ametumikia jukwaani kwa miaka 19, hivyo kwa kuwa umri umesogea na yeye ni mama mwenye mume na watoto (wake) wawili ameamua astaafu ili aweze kuitunza familia yake na maisha yake atayoyaendesha kwa ujasiriamali”, anasema Asha.

Lilian mwenyewe anaongeza kuwa siku hiyo atapanda stejini na kuonesha jinsi alivyo mahiri na mnenguaji mwenye kipaji kilichokuwa ndoto yake ya tangu alipokuwa binti na mtoto.

Amelaani pia tabia ya baadhi ya vijana kuwa na idadi kubwa ya wapenzi, lakini yeye anamshukuru Mungu kwamba ameweza kulipuka janga hilo ambapo sasa ni mke wa mtu.

“Asilimia kubwa ya wanenguaji wanatumia dawa za kulevya siyo kwa sababu ili wacheze vizuri jukwaaani, waliingia huko kwa kufuata mkumbo na mimi jambo hilo silifurahii. Linaniumiza sana”, anasema gwiji huyo anayenengua stejini kwa namna zote maridadi, kisha anaomba Mungu awasaidie ili kuondokana na janga hilo.

No comments:

 
 
Blogger Templates