Social Icons

Wednesday, June 6, 2012

KIINGILIO MECHI YA TAIFA STARS, GAMBIA 3,000

Baadhi ya wachezaji wa Timu ya Taifa ya Kilimanjaro Taifa Stars wakiwasili kwenye Uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere Dar es Salaam wakitokea Abdijan, Ivory Coast ambako walishiriki michuano ya kuwania kufuzu Kombe la Dunia dhidi ya Ivory Coast

Habari zote zimetolewa na Boniface Wambura,Ofisa Habari
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)

Kiingilio cha chini ya mechi ya mchujo ya Kombe la Dunia kati ya Tanzania (Taifa Stars) na Gambia (The Scorpions) itakayochezwa Jumapili (Juni 10 mwaka huu) Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam ni sh. 3,000.

Watazamaji watakaolipa kiingilio hicho ni watakaokaa kwenye viti vya rangi ya bluu na kijani ambavyo ni 36,693 kati ya jumla ya viti 57,558 vilivyopo katika uwanja huo wa kisasa. Kiingilio kwa viti vya rangi ya chungwa ni sh. 5,000.

Kwa upande wa VIP C watalipa sh. 10,000 wakati VIP B ni sh. 20,000. Kiingilio kwa jukwaa la VIP A ambalo linachukua watazamaji 748 tu ni sh. 30,000 kwa mechi hiyo itakayoanza saa 10 kamili jioni.

Tiketi zitaanza kuuzwa Jumamosi (Juni 9 mwaka huu) kuanzia saa 2 asubuhi kwenye vituo vya Mgahawa wa Steers ulioko Mtaa wa Ohio na Samora, Shule ya Sekondari Benjamin Mkapa, Soko Kuu la Kariakoo na Uwanja wa Taifa. Siku ya mechi pia mauzo yatafanyika katika vituo hivyo na baadaye kuhamia Uwanja wa Taifa.

GAMBIA YATARAJIA KUINGIA LEO DAR ES SALAAM
Timu ya Taifa ya Gambia (The Scorpions) inatarajia kuwasili nchini wakati wowote kuanzia leo (Juni 6 mwaka huu) tayari kwa ajili ya mechi dhidi ya Taifa Stars.

Kamati ya Maridhiano inayoendesha Chama cha Soka Gambia (GFA) hadi leo mchana ilikuwa haijatuma taarifa rasmi kwa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) juu ya ujio wake.

Lakini vyombo vya habari vya Gambia vimeripoti kuwa timu hiyo ikiwa na wachezaji 23 na viongozi tisa ilitarajiwa kuondoka huko leo kuja Dar es Salaam tayari kwa ajili ya mechi hiyo inayosubiriwa kwa hamu na washabiki wengi nchini.

Kwa mujibu wa Ofisa Habari wa GFA aliyekaririwa na vyombo vya habari vya nchi hiyo, Bakary Balder, msafara wa timu hiyo utaongozwa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Vijana na Michezo, Malang Jassey. 

Mbali ya Jassey, viongozi wengine katika msafara huo ni Ofisa Utawala wa timu Modou Sowe, Kocha Luciano Machini, makocha wasaidizi Peter Bonu Johnson na Lamin Sambou, Kocha wa makipa Alhagie Marong, mtaalamu wa tiba mbadala (physiotherapist) Pa Matarr Ndow, Mtunza vifaa Sanna Bojang na Daktari wa timu Kalifa Manneh.

Wachezaji ni Musa Camara, Abdou Jammeh, Momodou Futty Danso, Lamin Basmen Samateh, Ousman Koli, Pa Saikou Kujabi, Mustapha Kebba Jarju, Yankuba Mal Ceesay, Demba Savage, Saihou Gassama, Alieu Darboe, Momodou Ceesay, Pa Modou Jagne, Tijan Jaiteh, Bubacarr Sanyang, Christopher Allen, Musa Yaffa, Sulayman Marr, Mamut Saine, Hamsa Barry, Ali Sowe, Omar Colley na Saloum Faal.

                       TANZANIA YAPANDA VIWANGO VYA FIFA
Tanzania imepanda kwa nafasi sita kwenye orodha ya viwango ya Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) iliyotolewa leo (Juni 6 mwaka huu) na shirikisho hilo.
Kwa viwango vya Mei mwaka huu, Tanzania ambayo timu yake ya Taifa (Taifa Stars) inadhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager ilikuwa namba 145 hivi sasa imefika nafasi ya 139 ikiwa na pointi 214.

Mei 26 mwaka huu Taifa Stars ilicheza mechi ya kirafiki na Malawi na kutoka suluhu. Malawi yenye pointi 324 imeporomoka kwa nafasi tano kutoka ya 102 hadi 107.
Ivory Coast ambayo katika mechi yake ya mwisho Juni 2 mwaka huu iliifunga Taifa Stars mabao 2-0 imeporomoka kwa nafasi moja kutoka ya 15 hadi 16 ikiwa na pointi 943. Hata hivyo ndiyo inayoongoza kwa upande wan chi za Afrika katika viwango hivyo.
PROGRAMU YA TAIFA STARS KWA MECHI YA GAMBIA
JUMATANO JUNI 6
01.00 asubuhi Mazoezi- Uwanja wa Karume
10.00 jioni Mazoezi- Uwanja wa Taifa
ALHAMISI JUNI 7
10.00 jioni Mazoezi- Uwanja wa Taifa
IJUMAA JUNI 8
10.00 jioni Mazoezi- Uwanja wa Taifa
JUMAMOSI JUNI 9
04.00 asubuhi Mkutano na Waandishi wa Habari- Ukumbi wa TFF
11.00 jioni Mazoezi- Uwanja wa Taifa

No comments:

 
 
Blogger Templates