Social Icons

Monday, November 28, 2011

TWANGA PEPETA YADONDOSHA MAKOMBORA KUAMSHA SHEREHE ZA MIAKA 50 YA UHURU LONDON

Mcheza shoo  nyota na machachari wa bendi ya Twanga Asha  Saidi 'Sharapova' akiwa kazini 

Na Freddy Macha
African Stars Entertainment Tanzania(Aset) ambao wanajulikana kwa jina la “Twanga Pepeta” walikuwa kivutio cha sherehe za miaka 50 ya Uhuru London juzi Jumamosi. Kikosi hiki cha watumbuizaji maarufu wa Kibongo kilikaribishwa na Urban Pulse, Jestina George wakishirikiana na Ubalozi wa Tanzania mjini hapa.

Watanzania wa kila rika, nasaba na taaluma walifurika toka miji ya Leeds, Bristol, Birmingham, Northampton, Milton Keynes na vitongoji mbalimbali kufurahia vigongo vya bendi hili lenye makao makuu Mango, Kinondoni Dar es Salaam. Ukumbi wa Club 2000 Banqueting Suite ulioko nyuma ya uwanja maarufu wa Wembley ulishuhudia tafrija hiyo wakati viongozi rasmi wa serikali walipofungua tafrija wakicheza nyimbo maarufu za Kitanzania kama ule wa mwanamuziki Salum Abdallah (“Wanawake wa Tanzania” na “Tujenge Nchi Yetu”) marehemu alizoimba mara baada ya Uhuru mwaka 1961.
Viongozi waliojumuika walikuwa Naibu Waziri katika Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na serikali za mitaa, Mheshimiwa Aggrey Mwanri, Balozi wetu Uingereza, Mheshimiwa Peter Kallaghe, naibu wake Mheshimiwa Chabaka Kilumanga na Ofisa Habari ndani ya ubalozi,Mheshimiwa Amos Msanjila aliyehamasisha wageni kwa kunyofoa kinywaji cha “champagne” mahsusi kuzindua maadhimisho.
Akiwakaribisha wote Balozi Kallaghe alisema sherehe za miaka 50 ni idhinisho kuwa Tanzania ni nchi ya amani inayostahili kuwa fahari yetu sote.

“Waangalie Waingereza wanavyoorodhesha tarehe na mida ya majengo yao muhimu. Kutambua na kusherehekea muda kamili wa matukio ya jamii ni jambo muhimu na la kawaida,” alikumbusha kiongozi huyo na kupigiwa makofi.
Kutokana na maombi mengi ya washabiki Twanga Pepeta itafanya Show ya pili siku ijumaa Tarehe 2 Desemba 2011 katika mji wa Milton Keynes kwenye ukumbi wa Golden Lounge, Unit 35 Barton Road, Bletchley Milton Keynes. MK2 3UH
Show hii imeandaliwa na Urban Pulse wakishirikiana na Miss Jestina blog.


 Club 2000 palikuwa hapatoshi katika onyesho hilo la bendi ya The African Stars 'Twanga Pepeta International'(Picha zote zimetumwa na Urban Pusle)
                                                Kiboshoooooooo bila ya huyu hakuna kitakachonoga wala kueleweka.
 Mashabiki wa Twanga  wakijiachia kwa raha zao.
 Mheshimiwa Balozi wa Tanzania nchini Uingereza Peter Kallaghe aliyekuwa mgeni rasmi katika onyesho hilo  akitoast na wageni katika onyesho hilo la miaka 50 ya Uhuru ambapo bendi ya Twanga imetoa burudani.
 Mheshimiwa Chabaka  Kilumanga na Mchumba wake wakierebuka mangoma ya Twanga.
 Kiongozi wa bendi Luiza Mbutu Mamaa Brian  nyuma yake ni Kiongozi Msaidizi Sale Kupaza Mwana Tanga wakiwa jukwaani ambapo imesemekana kwamba wametoa shoo ya nguvu Usiku wa Jumamosi jijini London.
 Hawa ndiyo wanamuziki wa bendi ya Twanga ambao wako Ungereza katika ziara ya kusherehekea miaka 50 ya Uhuru.Wakiwa katika picha ya pamoja na viongozi na wenyeji wao
  Muimbaji kisiki wa bendi hiyo Hamisi Kayumbu Amigolas akiwa katika mzuka wa  kikazi zaidi na mnenguaji Asha Said a.k.a Sharapova.

No comments:

 
 
Blogger Templates