Social Icons

Tuesday, August 1, 2017

UMOJA WA ULAYA KUOKOA WASICHANA WASICHANA 3,738 KUKEKETWA NA NDOA ZA UTOTONI


Na Jacquiline Mrisho – MAELEZO
Jumla ya wasichana 3,738 wa Mikoa ya Mara na Geita wanategemea kunufaika na mradi wa Kuzuia Ndoa za Utotoni na Ukeketaji unaofadhiliwa na Umoja wa Nchi za Ulaya (EU) na kuratibiwa na shirika la Plan International kwa kushirikiana na mashirika ya CDF, NELICO pamoja na Molly”s Network.


Takwimu hizo zimetajwa leo na Mkurugenzi Msaidizi wa Shirika la Plan Tanzania, Gwynneth Wong wakati wa uzinduzi wa mradi huo uliofanyika katika ukumbi wa ofisi za Umoja wa Ulaya Jijini Dar es Salaam. Bi. Gwynneth amesema kuwa mradi huo ni moja kati ya miradi inayoratibiwa na shirika hilo ikisaidiana na Serikali ya Tanzania katika kuhakikisha haki za wasichana zinalindwa na hakuna msichana atakaeachwa nyuma kwenye nyanja za maendeleo hali itakayopeleka wasichana kuwa na haki sawa na wavulana.

“Tumeona kuna haja ya kuweka mradi mwingine utakaodumu kwa miaka mitatu wa uzuiaji wa mimba za utotoni na ukeketaji kwa mikoa ya Mara na Geita kwani mikoa hiyo imeonekana kuongoza kwa matatizo hayo hivyo tunaushkuru Umoja wa Nchi za Ulaya kwa kutoa jumla ya shilingi bilioni 1.4 kwa ajili ya kuendeshea mradi huu,”alisema Bi. Gwynneth.

Bi. Gwynneth ameongeza kuwa takwimu za mwaka 2016 za Utafiti wa Demographia na Afya unaonyesha kuwa ndoa za utotoni mkoani Mara ni asilimia 55 na kwa Geita ni asilimia 37 na ukeketaji kwa Mkoa wa Mara ni asilimia 32 kwa asilimia za kitaifa hivyo ni lazima kuanza na maeneo yaliyoathirika zaidi.


Kwa upande wake Balozi wa Umoja wa Ulaya, Roeland Van de Geer amesema kuwa umoja huo unatambua nafasi ya msichana katika jamii na nafasi ya baadhi ya mashirika yanayoshirikiana na Serikali katika kusukuma gurudumu la maendeleo kwa kuhakikisha haki sawa kwa wote.


“Sisi tunatoa fedha lakini nyie ndio watendaji hivyo tunawashukuru sana, lakini pia tunatakiwa tutambue kuwa maendeleo ya kudumu hayawezi kupatikana kwa kuwaacha wanawake nyuma kwa maana hiyo tunatakiwa tufanye juhudi za kuhakikisha tunaenda pamoja,” aliongeza Balozi Roeland Van de Geer.


Pia, Balozi huyo ameyashukuru baadhi ya mashirika yanayojitolea kufanya kazi ya kuhakikisha haki za msingi za binadamu zinalindwa na kuheshimiwa na ametoa wito kwa mashirika mengine kuendelea kusaidia maendeleo ya wasichana kwa sababu haki zao ndizo zinazovunjwa zaidi.


Mradi huo una malengo ya kuhakikisha wasichana wanaweza kuelewa haki zao na kuweza kutoa mawazo yao kwa jamii, kuhakikisha Serikali inasaidia wasichana kumaliza tatizo la ndoa za utotoni na ukeketaji.Kwa Mkoa wa Mara mradi utatekelezwa katika Wilaya ya Tarime ambapo utagusa jumla ya Kata tano na Geita mradi utagusa Kata 4.

No comments:

 
 
Blogger Templates