Social Icons

Thursday, May 18, 2017

MASHIRIKA YA KIMATAIFA YAOMBWA KUISAIDIA TANZANIA KUWAUNGANISHA RAIA WAPYA NA WATANZANIA WENGINE

Na Tiganya Vincent-Kaliua

Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiako wa Kimataifa, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashiriki katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Celestine Mushi ametoa wito kwa Mashirika Kimataifa na Umoja wa Ulaya kushirikiana na Serikali ya Tanzania katika kuwasaidia Watanzania wapya (waliokuwa wakimbizi wa Burundi) kuhakikishwa wanaunganishwa na jamii ya Watanzania mara baada ya kupata uraia.

Balozi Mushi ametoa kauli hiyo jana katika eneo la Ulyankulu wilayani Kaliua wakati alipokuwa na Ujumbe wa Mabalozi kutoka Nchi wanachama wa Umoja wa Ulaya ikiwemo Uingereza.

Alisema kuwa baada ya Serikali kuwapatia waliokuwa baadhi ya wakimbizi wa Burundi Uraia ni vema nchi hizo na Mashirika ya Kimataifa yakasaidia kuongeza raslimali mbalimbali ambazo zitaisaidia Serikali iweze kuwaunganisha vizuri raia hao wapya na raia wengine hapa nchini.

Balozi Mushi aliongeza fedha za Serikali pekee hazitoshi kukamilisha zoezi la kuwaunganisha raia hao kwasababu yapo mahitaji ya wananchi mengine hapo nchini yanayotegemeza hizo fedha kidogo inazokusanya kutokana na vyanzo vyake mbalimbali vya mapato na hivyo ni vema nao wakasaidia kwa upande wao.

Alisema kuwa kimsingi raia hao wapya wanakabiliwa na matatizo mbalimbali ikiwemo ukosefu wa maji safi na salama, uhaba wa vifaa tiba, zahanati , kutokuwa na miundombinu ya kutosha ya elimu na kukosa elimu ya kutosha kuhusu uzazi wa mpango.

Alisema kuwa kukosekana kwa elimu ya kutosha kumewafanya wakazi hao wawe na familia kubwa ambazo hawawezi wakati mwingine kuziwezesha katika huduma za jamii.

Balozi Mushi alisisitiza kuwa kutozingatiwa kwa elimu ya uzazi wa mpango kumelifanya eneo hilo kuwa na wananchi wanaozaliana kwa wingi kuliko maeneo mengine ya Mkoa wa Tabora jambo linalofanya huduma za jamii kuwa kidogo ukilinganisha na idadi ya watu wa hapo.

Alisema kuwa ni vema wadau wakaona ni wapi wanaweza kushirikiana na Tanzania katika kuwasaidia raia hao wapya katika kuondokana na matatizo mbalimbali yanayowakabili. Kwa upande wa Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Kaliua Dkt. John Pima alisema kuwa wastani wa raia kuzaana katika eneo la Ulyankulu ni asilimia 5.4 na hivyo kufanya kuwepo na idadi ya watu wengi katika eneo moja ambao hawawiani na huduma za jamii zilizopo.

Alisema kuwa hatua inasabaisha kuwepo kwa uhaba wa vyumba vya madarasa ,hatua iliyoilazimu Halmashauri hiyo kujaribu kuwahamishia katika maeneo mengine watoto hao ili wapate elimu. Dkt. Pima aliongeza kuwa kuhusu elimu ya uzazi wa mpango wamekuwa wakijitadi kuitoa lakini bado kasi ya uzalianaji ni kubwa na hivyo juhudi zaidi zinahitajika.

Naye Mkurugenzi Msaidizi kutoka Idara ya Huduma ya Wakimbizi Suleman Mziray ujumbe wa Mabalozi wa Umoja wa Ulaya umekwenda Ulyankulu ili kujionea hali halisi na kuangalia jinsi gani wanaweza kuisadia Serikali ya Tanzania katika kutengamanisha waliokuwa Wakimbikizi ambao wapata uraia na Watanzania wengine.

Alisema kuwa mabalozi hao wamekuwa na Umoja wao unajulikana kama Solutions Alliance ambao lengo lake ni kutafuta suluhusho la kuduma kwa wakimbizi.

Mziray aliongeza kuwa ziara ya Mabalozi hao ilikuwa muhimu ili waweze kuona wapi wanaweza kusaidia katika kuboresha kundi hilo. Aidha , alitoa wito kwa Watanzania hao wapya kuanza kuangalia uwezekano wa kuhamia katika maeneo mengine ya kuishi ili kuepuka tatizo la ukosefu wa huduma za jamii kama maji na elimu.

Serikali ya Tanzania imetoa uraia kwa wakimbizi wa Burundi 162,000 walioishi nchini 1972 na kuwa Watanzania. Ujumbe huo wa Mabalozi wa Umoja wa Ulaya nchini umesema utakwenda kukaa na baadaye ndio utatoa majibu iwapo wanaweza kusaidia na ni eneo gani.

No comments:

 
 
Blogger Templates