Social Icons

Friday, December 16, 2016

MKURUGENZI WA JAMII FORUM APANDISHWA KIZIMBANI LEO



Mkurugenzi wa mtandao wa JamiiForum, Maxence Melo amepandishwa kizimbani kwenye Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu leo akikabiliwa na makosa manne likiwemo la kuzuia taarifa za upelelezi kwa jeshi la polisi.

 Melo amepandishwa kizimbani ikiwa ni siku nne tangu alipokamatwa na Polisi, kisha kuzuiwa kupewa dhamana.

 Melo alifikishwa mahakamani hapo saa 2:50 asubuhi akiwa chini ya ulinzi mkali wa Jeshi la Polisi akitokea kituo Kikuu cha Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam. 

 Mara baada ya kufikishwa mahakamani hapo, Melo aliyevalia shati la drafti jeusi na suruala yenye rangi ya kahawia aina ya ‘Kadeti’ na malapa ya bluu alipelekwa kwenye chumba cha mahabusu. Baada ya kukaa mahabusu, alitolewa na kupandishwa kizimbani mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi, Thomas Simba saa 9:47 asubuhi.


Hata hivyo, hadi anafikishwa ndani ya chumba cha mahakama hakukuwa na watu wengi kutokana na wengi wao kutokuwa na taarifa kwamba angefikishwa mahakamani hapo kwa haraka namna hiyo. 

 Mara baada ya kuingia kwenye chumba hicho cha mahakama, alikabidhiwa hati ya mashtaka yenye makosa yanayomkabili. Wakili wa Serikali Mwandamizi, Mohamed Salum alieleza kuwa Melo anakabiliwa na kosa moja la kuzuia upelelezi. 

Alidai kuwa katika tarehe tofauti kati ya Aprili 1 na Desemba 13, mwaka huu maeneo ya Mikocheni wilaya ya Kinondoni jijini Dar es Salaam, akiwa Mkurugenzi wa Jamii Media Co Ltd unaoendesha mtandao wa Jamiiforums, 

Akijua kwamba Jeshi la Polisi lipo kwenye uchunguzi wa makosa ya kimitandao zilizochapishwa kwenye mtandao wake  , kinyume na sheria alishindwa kutoa ushirikiano na kuzizuia taarifa za mtandao huo. 

 Baada ya kusomewa shtaka hilo, Melo alikana kuhusika na kosa hilo
Wakili Mohamed anaomba kupangiwa tarehe nyingine kwa kuwa upelelezi wa shauri hilo unaendelea. 


 Hata hivyo, wakili wa utetezi Jebra Kambole aliiomba mahakama kumpa masharti ya dhamana Melo kwa kuwana kosa hilo linadhaminika na ana haki ya kupata dhamana kama ilivyo kwa Watanzania wengine.

 Hakimu Simba, alitoa masharti ya kuwepo kwa wadhamini wawili waaminifu watakaosaini bondi ya Sh.milioni 10 kwa kila mmoja, ambapo Melo alifanikiwa kuyatimiza. 

 Baada ya hapo, Hakimu Simba aliahirisha kesi hiyo hadi Januari 29, mwaka huu kwa ajili ya kutajwa. 

 Kesi ya pili Wakati ndugu na jamaa wakiwa na hamu, msubiri Melo kukamilisha taratibu za dhamana, ghafla waliona akikamatwa na kupelekwa kwa hakimu mwingine.

 Hatua hiyo iliwaduwaza wengi, kutokana na uamuzi huo wa upande wa serikali kumkamata na kumfikisha mbele ya hakimu mwingine ambaye ni Victoria Nongwa. 

 Akisomewa mashtaka mengine Mbele ya Hakimu Mkazi wa mahakama hiyo, Victoria Nongwa wakili wa serikali Mohamed Salum alidai kuwa mshtakiwa anakabiliwa na makosa mawili. 

 Wakili Salum alidai kosa la kwanza alilitenda Desemba 9 na 13 mwaka huu katika maeneo ya Mikocheni Kinondoni jijini Dar es Salaam ambapo akiwa Mkurugenzi wa Jamii Media Co. Ltd iliyosajiliwa chini ya kifungu 212 RE cha mwaka 2002 chenye namba 66333, anaendesha mtandao wa Jamii Forums bila kusajiliwa hapa nchini kwa mujibu wa sheria za mtandao na masuala ya posta. Kosa jingine la kuzuia upelelezi kwa Jeshi la Polisi alilitenda Januari 26 na 13 mwaka huu, ambapo akiwa Mkurugenzi wa Jamii Media Co Ltd unaoendesha mtandao wa Jamiiforums, akijua kwamba Jeshi la Polisi lipo kwenye uchunguzi wa makosa ya kimitandao zilizochapishwa kwenye tovuti yake, kinyume na sheria alishindwa kutoa ushirikiano na kuzizuia taarifa za mtandao huo. Baada ya kusomewa shtaka hilo, Melo alikana kuhusika na kosa hilo. Wakili Mohamed anaomba kupangiwa tarehe nyingine kwa kuwa upelelezi wa shauri hilo unaendelea. 

Hakimu Nongwa alisema mashkata yote yanayomkabili yanadhamana na kutokana na hilo anatakiwa kujidhamini mwenyewe na kupata wadhamini wawili ambao kila mmoja atatakiwa kuwa hundi la milioni moja. 

 Masharti hayo yalikamilika hivyo mshitakiwa aliachiwa huru kwa sharti ya kutoruhusiwa kutoka nje wa mahakama bila ruhusa. Kesi ya tatu Akiwa mbele ya Hakimu Mkazi, Godfrey Mwambapa wakili wa Serikali Mohamed Salum alieleza kuwa mshtakiwa huyo anakabiliwa na kosa moja la kuzuia taarifa za upelelezi. 

 Katika kesi hiyo iliyopewa namba 456, Wakili Salum alieleza kuwa mshtakiwa alitenda kosa hilo katika tarehe tofauti kati ya Aprili 1 na Desemba 13, mwaka huu. Inadaiwa akiwa maeneo ya Mikocheni wilaya ya Kinondoni jijini Dar es Salaam, akiwa Mkurugenzi wa Jamii media inayoendesha mtandao wa Jamiiforum, Inadaiwa akijua kwamba Jeshi la Polisi linafanya uchunguzi wa makosa ya taarifa za kimtandao ya elektroniki kupitia tovuti yake, alishindwa kutoa taarifa na kuzuia uchunguzi wa tovuti hiyo. Baada ya kusomewa shtaka hilo, Melo alilikana. 

Wakili wa Salum aliomba shauri hilo liahirishwe hadi tarehe nyingine kwa kuwa upelelezi kesi hiyo bado haujakamilika. Hata hivyo, wakili Kambole alieleza kuwa shtaka hilo linadhaminika na anaomba mteja wake adhaminiwe. Hakimu Mwambapa alitoa masharti ya dhamana ya wadhamini wawili watakaosaini bondi ya Sh.milioni 5 kwa kila mmoja. 

 Hata hivyo, Melo alirudishwa lumande baada ya kushindwa kutumiza masharti baada ya mdhamini mmoja kuchelewa kuwasilisha barua ya udhamini. Kutokana na hatua hiyo, Hakimu Mwambapa ameahirisha kesi hiyo hadi Desemba 29, mwaka huu, huku akisema endapo mshtakiwa huyo akitimiza masharti atatolewa muda wowote. 

 Nje ya mahakama Akizungumza na waandishi wa habari jana nje ya mahakama, Mwanasheria Mwandamizi Mkuu wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), Johannes Kalungula mamlaka hiyo haitauvumilia mtandao wowote ambao utafanya kazi kinyume cha sheria na taratibu za nchi. Alisema hawatasita kuufungia mtandao utakaobainika kuwa umekiuka sheria za mtandao na masuala ya posta iliyopo nchini kwa kuficha waarifu na kuhusu kutumika kama kichaka cha kusema mambo ya uongo.

 “Sheria za nchi yetu zipo wazi sana juu ya mambo mbalimbali na endapo itabainika kuwa kuna mtandao ambao umekiuka sheria ya mtandao na masuala ya posta iliyopo nchini mara moja tutaufungia wala hatutasitasita, lakini tumebaini kuwa hipo mitandao sasa inatumika vibaya kwa kufisha wahalifu lazima tukemee na tumeanza na mkurugenzi huyo ambaye tumemfikisha mahakamani,” alisema. 

 Aidha alisema serikali kwa ujumla haizuii matumizi ya mtandao ili kinachozuia ni matumizi mabaya. Naye wakili upande wa utetezi Jebla Kambole alisema walichokikuta mahakamani jana wala hawakutegemea kwani staka liliokuwa likimkabili limegawanywa kwa mahakimu watatu tofauti. 

 Alisema kugawanywa huko kumewafanya kushindwa kuwaandaa wadhamini wengine ambao walikuwa wakihitajika kumzamini mshatakiwa jambo lilosababisha hadi kushindwa kuachiwa na kurudishwa rumande

. “Kutokana na kugawanywa kwa kesi hii imetuwia vigumu sisi kupata wadhamini kwa haraka ambao wangeweza kutimiza vigezo na imesababisha tulipofika kwa Hakimu wa mwisho tukakosa mdhamini na hakimu kuamuru mshtakiwa kurudisha rumande mpaka masharti yatakapokamilika,” alisema..

No comments:

 
 
Blogger Templates