Social Icons

Monday, September 5, 2016

RC KILIMANJARO AINGILIA KATI SUALA LA WANAFUNZI KUPEWA MIMBA

Paul Mruma, Rombo.

Sakata la Wanafunzi 60 wa shule za Sekondari wilayani Rombo mkoani Kilimanjaro kupewa mimba ndani ya Januari hadi Agosti mwaka huu limechukua sura mpya baada ya mkuu wa mkoa wa Kilimanjaro, Said Meck Sadick kuingilia kati na kuwataka Wazazi kuacha tabia ya kumalizana na wanaume wanaofanya vitendo hivyo majumbani na badala yake wawafikishe katika vyombo vya sheria.

Sadick alitoa kauli hiyo alipofanya ziara katika wilaya hiyo na kuzungumza na Wananchi wa Rombo katika soko la Tarakea ambapo alisema kuwa, vitendo hivyo vya kuwapata Wanafunzi wa kike mimba vimekuwa vikikidhiri kwa wingi wilayani hapo huku Wananchi wamekuwa wakimalizania majumbani badala ya kuwafikisha polisi.

Alisema kuwa, katika zoezi la upimaji watoto wa kike kwa shule za sekondari awamu ya kwanza iliyofanyika Juni mwaka huu jumla ya Wanafunzi 24 waligundulika kuwa ni wajawazito lakini katika hali ya kushangaza Wanafunzi walipoenda likizo ya mwezi wa sita waliporudi walipimwa tena ambapo Wanafunzi wapya 36 waligundulika ni wajawazito.

“Vitendo vya ujauzito kwa Wanafunzi wilaya ya Rombo inaongoza katika mkoa wangu ndani ya miezi miwili tu Wanafunzi 36 wamegundulika kuwa ni wajawajito tena idadi hii inaweza kuongezeka kutokana nab ado shule mbili hazijapimwa kutokana na kuishiwa kwa vifaa halafu hakuna hata kesi moja iliyoripotiwa polisi hii ni aibu” alisema Sadick.

Mkuu huyo wa mkoa alisema kuwa, watoto hao wamekuwa wakiachishwa shule kutokana na kupata ujauzito ambapo ni hasara kubwa kwa Serikali kwa sababu ndio wataalam wa badae, na viongozi wa Taifa wa badae lakini kwa sasa hawapo shuleni.

Alisema kuwa, zoezi hilo la upimaji mimba kwa Wanafunzi limefanywa kwa makusudi kwa sababu wanapojulikana mapema ni rahisi kuwajua wale waliowapa mimba hizo mapema ili waweze kuchukuliwa hatua za kisheria na kuwataka Wazazi kuacha tabia ya kuwaficha wanaume wanaofanya vitendo hivyo.

“Kuna mila ambazo zimepitwa na wakati mwanaume kakuaribia mtoto wako anakuletea majani mnayoyaita kwa jina la masala alafu etu mnamsamehe hii sio mila nzuri imepitwa na wakati kumbuka huyu mwanaume kamuaribia binti yako maisha na wala hatamuoa bali nyie wazazi ndi mtapata jukumu la kumlea”alisema Sadick.

Katika hatua nyingine mkuu huyo wa Mkoa alisema kuwa, wilaya hiyo ya Rombo inaongoza pia katika vitendo vya ubakaji vinavyosababishwa na ulevi, ushirikina ambapo wamekuwa wakiwabaka watoto walio chini ya umri wa miaka mitano ili kupata mali. Ikumbukwe kuwa katika taarifa iliyotolewa na mkuu wa wilaya ya Rombo, Agnes Hokororo ilisema kuwa, Wanafunzi hao wamekuwa wakipewa mimba na madereva bodaboda pamoja na Noah ambapo wamekuwa wakiwapa lifti na badae kuwarubuni kwa vitu vidogo dogo kama chipsi kuku na mayai.

No comments:

 
 
Blogger Templates