Social Icons

Tuesday, August 16, 2016

ORIGNAL COMEDY MIKONONI MWA POLISI NI KWA KUVAA SARE ZA POLISI KWENYE HARUSI YA MASANJA MKANDAMIZAJI



Katika siku za hivi karibuni, kumejitokeza  tabia kwa baadhi ya watu wakiwemowasanii watu wengine mmoja mmoja kutumia mavazi yanayofanana na sare za Majeshi ya Ulinzi na usalama hapa nchini likiwemo Jeshi la Polisi katika shughuli zao za kisanii au katika kazi mbalimbali, Jambo ambalo ni kinyume cha sheria,kanuni na taratibu za Nchi. 

Kwa mujibu wa Sheria ya kanuni za makosa ya Jinai, sura ya 16 na  marejeo  yake ya mwaka 2002,  kifungu cha 178 (1)  na  (2) kinachozungumzia makosa dhidi ya  sare za majeshi ya ulinzi na usalama,  kinabainisha  wazi kuwa ni kosa kisheria kwa mtu yeyote ambaye siyo mtumishi wa majeshi ya ulinzi na usalama kuvaa mavazi yanayotumiwa au kushabihiana na sare za majeshi hayo  bila kibali kutoka kwa  Mhe.Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Kufuatia  kitendo kilichofanywa na kundi la kisanii la “ Original Comedy” kuvaa mavazi yanayoshabihiana na sare za Jeshi la Polisi,Jeshi la Polisi Kanda Maalumu ya Dar Es Salaam linachukua  hatua za kisheria dhidi ya wasanii hao.

Aidha Jeshi la Polisi nchini, linatoa onyo kali kwa mtu ama kikundi chochote kuacha kutumia  mavazi yanayofanana na sare zinazovaliwa  na  majeshi ya ulinzi na usalama hapa nchini  na atakayebainika hatutasita kuchukua hatua kali za kisheria dhidi yake.

Jeshi la Polisi  linatoa rai kwa wale wote wenye mavazi yanayoshabihiana na sare za majeshi ya
ulinzi na usalama  kuzisalimisha mara  moja katika vituo vya Polisi vilivyokaribu nao.

Imetolewa na:
Msemaji wa Jeshi la Polisi.
Advera John  Bulimba – Kamishna
Msaidizi wa Polisi (ACP)

No comments:

 
 
Blogger Templates