Social Icons

Thursday, September 3, 2015

IMETOSHA MUSIC AND LAUGHTERS NIGHT


Nikianza na neno la shukrani, naomba nizitoe za dhati kwa kunivumilia, na kufanya nami kampeni ya Imetosha katika mazingira magumu sana katika awamu ya kwanza. Hii ni kutokana na ugeni katika uendeshwaji wa taasisi pamoja na uhalisia wa safari za kiharakati, mara nyingi wanaofika safari huwa ni wachache, lakini nyie hamkuwahi kukata tamaa katika kuniunga mkono.

Awamu ya kwanza ya kutambulisha taasisi na misimamo yake imefanikiwa, na sasa tunaenda katika awamu ya pili, ambapo baada ya kufanya matembezi, na kampeni mbali mbali ndogondogo, tulifanikiwa kwa kuungwa mkono na taasisi rafiki na azma ya kwanza ilikuwa ni kukiunga mkono kituo cha Buhangija kilichopo Shinyanga.
Lakini baada ya mimi binafsi kama muasisi na mwenye wazo, kufikiri kwa kina kuhusiana na Shinyanga, ambako kiukweli mazingira yake hayajathibitika kuwa salama, na pili kuwa ni kituo cha serikali, nilikuja na wazo la Taasisi kuwa na kijiji cha mfano ambacho, pamoja na kuhifadhi watu wenye ualbino na wasio na ualbino bali pia kiwe kituo cha uzalishaji mali, ambacho kitawakomboa watu wenye ualbino katika ile dhana na kuomba omba, na kuwa wachangiaji rasmi wa pato la taifa kwa kufanya biashara ya kilimo na ufugaji.
Hivi ninavyoongea tayari tumeshatoa malipo ya awali kwa Mzee idd Shemdoe wa huko Bumbuli, Lushoto, mkoani Tanga ambaye amekubali kuiuzia taasisi shamba la Mikahawa lenye ukubwa wa ekari 50. Hapo taasisi ina mpango wa kufungua kituo kitakachoitwa Santa Lucia, Safe House and Estate.
Eneo litatumika kwa kilimo, ufugaji, pamoja na elimu, kwa maana ya shule kubwa inayofundisha kwa mtaala wa kimataifa, lengo likiwa ni kuwawekea watu wenye ualbino vitega uchumi ambacho vitasababisha wao na taasisi yao kutowapigia wafadhili magoti mara kwa mara na badala yake kuwa sehemu ya watatuzi wa matatizo ya kijamii yanayoiklumba nchi.
Kaka na dada zangu, kuwa na eneo tu haitoshi, na safari ya kuifikia ndoto hii ni ndefu inayochukua muda mrefu kuikamilisha. Mimi naiamini kwa sababu tu nina nia na nimedhamiria kuifanya kama sehemu ya ndoto zangu za kimaisha.
Nachukua nafasi hii kuwaomba kunisaidia kushiriki katika shughuli mbali mbali nitakazokuwa nazifanya katika kutunisha mfuko wa taasisi, na hapa naileta kwenu shughuli ya Music and laughetrs, ambayo Orijino Komedi wamekubali kuwa wenyeji huku muziki nao ukichukua sehemu kubwa ya shughuli.

Hii itakuwa Septemba 11, naomba muwahimize wadau kadri muwezavyo wajitokeze kwa wingi kutuunga mkono kwa umoja wetu.

Mungu ibariki tanzania Mungu aubariki umoja wetu. 

No comments:

 
 
Blogger Templates