Social Icons

Friday, July 3, 2015

KILICHOMPONZA STEVE NYERERE HIKI HAPA

SIKU chache baada ya msanii wa vichekesho, Steve Mengele ‘Steve Nyerere’ kupigwa ‘stop’ kuendelea na mkutano wake wa hadhara Kinondoni, jijini Dar es Salaam, kilichomponza kimeanikwa.
Msanii huyo Juni 28 aliitisha mkutano wa hadhara Kata ya Bwawani kuhamasisha vijana kujiandikisha katika daftari la wapiga kura, lakini akiwa jukwaani Mwenyekiti wa CCM Tawi la Bwawani, alishika kipaza sauti na kutangaza kuwa amepokea amri kutoka ngazi za juu kuvunja mkutano huo, huku Steve Nyerere akibaki amepigwa butwaa.
Habari kutoka ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Kinondoni, zinaeleza kuwa msanii huyo alikiuka taratibu kwa kuutumia mkutano huo kutangaza nia kugombea ubunge huku wakati ukiwa bado haujafika na jimbo hilo likiwa na Mbunge wa CCM, Idd Azzan.
Chanzo hicho ambacho hakikupenda kutajwa jina kwa kuwa si msemaji rasmi wa chama, kilisema Steve Nyerere kama Kamanda wa Vijana wa Kata ya Bwawani, alikuwa sahihi kuhamasisha vijana  kujiandikisha kwenye daftari la mpiga kura, lakini kosa kubwa alilolifanya ni kutangaza nia.
“Kosa lililomponza na ambalo anaweza hata kushitakiwa kichama, ni kuutumia mkutano huo kutangaza nia, tena kwa kuongozana na msafara wa magari huku yakiwa na picha za kuhamasisha zikiwa na ujumbe: ‘Twende na Steve’, huku mwenye jimbo yupo... Endapo atamshitaki, atakuwa katika wakati mgumu kisiasa,” alisema kiongozi huyo.
Baadhi ya wanasiasa wakongwe  walieleza kwamba kitendo chake cha kuitisha mkutano wa hadhara na kuweka mabango ya picha zake si sahihi, kwa sababu wakati wa kutangaza nia na kuanza kampeni bado.
Mengele ambaye pia ni msanii wa filamu, alijizolea umaarufu kwa vichekesho na kipaji cha kuigiza sauti ya Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere na viongozi wengine mbalimbali. 

No comments:

 
 
Blogger Templates